Sunday, April 14, 2019

MFUNGWA HURU

_*NUSU ZUZU,NUSU ZEZETA*_

Akili nusu zezeta, nusu imekuwa zuzu, umeizuzua
Mwili umenizorota, mwembamba kama kauzu, umejikondea
Moyo unanitukuta, tuu! tuu! unajuzu, umeuonea


Miguu hafurukuta, imeingia kibibi, haina hisia
Tumbo linanisokota, umeisha ujanabi, umeshakimbia
Leo hii wanisuta, huniti tena hababi, yako kutumia


Huba kwako limekata, thamani 'mepukutika, ulonipatia
Kuna jambo ulifata, leo umenifutuka, hukua na nia
Ipo siku nitapata, mrembo kukufunika, alietimia


Uchungu umenipata, hadi haya kuandika, jua naumia
Shauri tulolikata, kuwa sote tutafika, hadi kwenye ndoa
Ni ruya yenye utata, na zuzu nimezuzuka, bora kujifia


Funzo nimeshalipata, kwako nilifanya kosa, sitalirejea
Nenda na mimi 'tapata, mzuri asie visa, na mbaya tabia
Amba mimi ni zezeta, na zuzu mtoa pesa, niko safi nia



_*Othman Ame Hamza*_
*_Mfungwa huru_*
0776820608
othame10@gmail.com

No comments:

Post a Comment